Monday

Mume wangu anatereza nje na "dada" zake na kuzaa ovyo, nifanye nini?


"Dada Dinah,Salaams.

Naona nianze moja kwa moja matatizo yangu. Mimi ni mwanamke umri miaka 38, nimeolewa miaka mitatu iliyopita, sina mtoto. Ninaishi na mume wangu pamoja na binti wa mume wangu ambaye anasoma boarding.


Tatizo kubwa ni kuwa nimeshindwa kumzalia mtoto mume wangu na hivyo ume wangu kazaa na housegirl wetu. Kabla hajampa ujauzito, aliomba nimfukuze akidai hana adabu. Baadaye nikaambiwa na majirani kuwa housegirl wetu ana mimba. Sikujua ni ya nani hadi hapo baadaye.


Baada ya muda nikagundua kuwa mume wangu anatembea na msichana jirani aliyekuwa akimuita dada kwa vile wanatoka sehemu moja. Dada huyo alikuwa akija kututembelea na wakati mwingine akitusaidia kazi wakati mimi nikisafiri. Kazi yangu ni ya kusafiri na baadaye nikahamishiwa Wilayani kabisa.


Kurudi kwangu nyumbani ni siku za weekend tu.Kumbe yule dada akawa anakuja kulala na mume wangu usiku. Nikaambiwa na majirani. Nilipomuuliza kama kawaida alikataa. Yule mwanamke baada ya kuona nimegundua amehama mkoa na kuhamia Dar.


Hivi karibuni nimetumiwa sms na msichana akiniambia kuwa ana mimba ya mume wangu na kuwa kaipatia nyumbani kwangu kwenye kitanda changu na kuwa eti nisubiri kuletewa watoto. Nilipofuatilia nikagundua kuwa huyo msichana ni mwanafunzi wa Sekondari na wanatokea sehemu moja pia na mume wangu.


Nilipomuuliza mume wangu alikanusha kama kawaida. Lakini baadaye nikapata taarifa kuwa mume wangu kampiga sana yule msichana hadi kulazwa Hospitali kwa kuwa eti kanitumia sms. Nilipomuuliza alikubali, halafu baadaye alikanusha akidai kuwa ingekuwa ni stori ya kweli basi angeshitakiwa police.


Kweli mambo ni mengi, mojawapo likiwa la mume wangu kutopenda kabisa mimi kugusa simu yake. Nilishakuta sms za wanawake wawili kwenye simu yake, mmoja ninayemfahamu. Hata nikiamka kujisaidia usiku, yeye anashituka akihofia simu zake zisiguswe. Mume wangu anao marafiki wengi wa kike yeye akiwaita ni dada zake na wengi wa kabila lake la Wapare, ambao wengine ndio hao anaotembea nao.


Sasa mimi sielewi hili kabila, nimegundua kuwa ni Malaya sana, hadi najuta. Mimi nafanya kazi na kipato changu ni kikubwa kuzidi cha mume wangu. Namnunulia nguo nzuri anapendeza, nimemsaidia kumjengea nyumba mama yake na sasa tunajenga ya kwetu. Nampenda sana mume wangu na yeye anadai kunipenda.


Kutokana na hali hiyo afya yangu Kisaikolojia imeharibika, naombaeni ushauri wenu. mngekuwa ni nyie mngefanya nini"?

Pages