Friday

Ngono kabla ya ndoa ni tofauti na nje ya ndoa!

Sema wewe, mambo yako?
Kufuatia Somo moto kutoka kwa M3 napenda kutoa maelezo yangu ktk mgawanyiko na leo naanza kama kichwa cha habari kinavyosomeka hapo juu.


Nisingependa kuegemea sana kwenye maandiko ya dini mbili ninazo amini ili kuepuka kuigawa jamii ya wasomaji wangu, ila napenda kukumbusha tu kuwa kuna maandiko yenye maana sawa na “mjizuie/msioe lakini mkishindawa kutokana na tamaa/mahitaji ya mwili basi na muoe, mwili wa mwanamke sio wake pekee bali pia ni wa mume wake hali kadhalika wa mwili wa mwanaume sio wake pekee bali ni wa mkewe”.

Hivyo ukiangalia kwa undani hapo utagundua kuwa nia na madhumuni ya kuoa/olewa ni kungonoana alafu swala la kuzaliana ni matunda ya tendo hilo takatifu na mengine yanafuata(nitalizungumzia hili nkirudi).

Swala la kusubiri ngono mpaka ufunge ndoa linasisitizwa na dini mbili nizijuazo mimi lakini pia Miiko na Mila mbali mbali zina amini nakusisitiza hilo wakati baadhi yao ngono inafanywa mara tu kijana au binti anapobalehe/kua/Pevuka na ngono hiyo hufanywa kati ya binti/kijana na ndugu wa mwanzo wa familia kama vile baba/binamu/shangazi(wanakufungua kabla hujaenda kuolewa/oa).

Tunapozungumzia swala la kutokufanya ngono kabla ya ndoa kwa kufuata Miiko au Imani zetu basi ni vema kama tukawa tunafanya kila jambo linalotakiwa kwenye Miiko na Imani tunazoamini, lakini wangapi wanasubiri ngono mpaka ndoa na wanafanya kila lililojema linalosisitizwa kwenye vitabu vya imani zao?


Nakubali kuanzia miaka ile mimi nakua (90s) kumekuwa na mlipuko wa watu kufanya ngono kabla ya ndoa, hali iliyo sababishwa na inaendelea kusababishwa na mambo mbali mbali likiwemo swala zima la uchumi, kubaki shuleni kwa muda mrefu, kugundulika kwa utamu wa ngono kwa wanawake wengi kwamba ngono sasa sio chanzo cha kuzaliana tu bali ni sehemu ya kufurahia ujinsia wetu tofauti na zamani ambapo lengo na madhumuni la tendo hili lilikuwa ni kumpa raha mume na kuendeleza vizazi.


Kabla ya hapo wanawake ndio walikuwa wakijitahidi kusubiri na kuifanya ngono au kushiriki tendo hili baada ya kuolewa tofauti na wanaume kwani wengi walikuwa wakioa wanawake bikira baada ya wao kuwa na uzoefu kitu ambacho mimi nakiona kama dhuluma (hihihihihihihi....ndio je!).


**Sababu kubwa inayotufanya ngono ifanywe kabla ya ndoa.

Tofauti na miaka ile, sasa vijana wengi wake kwa waume tunaamua kurekebisha maisha kwanza alafu ndio ndoa ifuate, sasa unapofikia umri mkubwa wa miaka 24 mpaka 35 inakuwa ngumu sana kwako wewe kuendelea kutafuta maisha kielimu na kiuchumi na kuidharau mahitaji yako ya mwili na roho (ngono na mapenzi) ambayo katika kipindi hiki ndio hupamba moto (minyenyere mpaka kwenye kope na moyo nao unahitaji kujazwa mapenzi).


Hapa ndio wengi tunaamua kuwa na wapenzi wa kudumu na kuifanya ngono kama ifuatavyo (kwa uhuru) hali inayotufanya wengi tutulie kiakili na baada ya hapo kufunga ndoa ili tuweze kushirikiana na kufanikisha malengo yetu kama wapenzi na mungu akijaalia tunaongeza kizazi.

Vijana wachache wanajitahidi kuepuka mimba wakati wa mahusiano yao ya kimapenzi ili kutosababisha watoto nje ya ndoa wakisubiri kutekeleza tukio hilo muhimu ktk maisha ya kila mwanadamu hasa wale wanaoendeleza Imani zao za kidini.

Ufanyaji huu wa ngono unaitwa ngono kabla ya ndoa ambao ni tofauti na ngono nje ya ndoa(kuchoropoka/cheating).

Natambua wengi huwa mnachanganya hapa!

Ikiwa unalolote unataka kuongezea kuhusiana na nilichokisema kwa faida ya wasomaji wengine, usisite kufanya hivyo.

Shukurani kwa ushirikiano.

Wednesday

Umri kwenye mapenzi-Ushauri.

"Dada Dinah, hili la leo ni dukuduku la kijana mmoja, mwenye umri wa miaka 19. Kijana huyu analalamika kwani wazee wake `hawamtendei haki' kama alivyodai.
`Kijana kamtunuku `kikongwe'' kauli zimezagaa mitaani.


Sio kikongwe kwa umri, ila vijana wenzake mitaani wameamua kukuza, kwani `limama' analolitaka limemzidi karibu mara mbili. Samahani kwa kumuita huyu mama `limama' ila nimenogeza kwasababu umejazia sio mchezo! 'Unajua wazazi wangu hawaelewi kwanini nimempendea yule `mother', mimi sikubali mpaka nimuweke ndani' alilalamika huyu kijana.


Sasa Dinah, sijui tutamsaidiaje huyu kijana, kwani huenda anakile kinachoitwa `infatuation' au kimuhemuhe cha mapenzi, au ndio kama walivyovumisha ndugu zake kuwa huenda ametengenezwa. Na huenda kayapata mapenzi ambayo anahisi hayawezi kuyapata kwa mwanamke mwingine, au kweli kampenda, huwezi jua!

Je kuna madhara yoyote kwa kijana kama huyu kumuoa mama aliyemzidi umri karibu mara mbili ya umri wake? Kwa wanaume inawezekana, hiyo ipo dhahiri! Lakini nashangaa kwa wanawake inakuwa `issue'

Nikilipeleka swali hili kiutu uzima zaidi, je ipo raha gani kijana kama huyu ataipata kwa mama huyu, tukizingatia kuwa jinsi umri unavyokwenda ndivyo hali hasa ya `uke' inavyokwisha! Sijui kama nimekosea hapa! Na kwa mfano ndio wameoana, jinsi gani `wafanye' ili wasipishane kimalovu.

Ahsanteni
Emu-three".

Jawabu: M3 asante kwa kulileta swali lako mahali hapa,nafikiri neno Jimama (sifa) lingependeza zaidi kuliko limama (kashfa). Kama ulivyosema kwa wanaume inawezekana lakini inashangaza kwanini kwa wanawake inakuwa "big deal" hii inawezekana kabisa kuwa ule mfumo dume unamizizi miongoni mwa wanajamii sio wa Bongo tu bali Duniani kote.

Kisheria (Tz) na Kimila kijana anaruhusiwa kuoa akiwa na miaka 18 hivyo huyu bwana mdogo anapaswa kufuata moyo wake na kutosahau akili yake (kuwa makini na uhakika wa kile anachotaka kukifanya).

Kama wazazi na ndugu wa karibu wanapaswa kumshauri na kumtahadharisha lakini sio kumtisha au kumlazimisha ili kuachana/ua uhusiano kwa vile tu mtu anaempenda ni mkubwa sana kwake.

Mapenzi ni hisia alizo nazo mtu juu ya mtu mwingine na hazina uhusiano wowote na umri, muonekano, mali, umbile na vitu vingine ambavyo watu wengi huvihusisha na mapenzi kimakosa. Penzi hujitokeza mahali popote na wakati wowote juu yamtu yeyote, hakuna mtu anapenda kumpenda fulani bali inatokea tu kuwa "umefika bei" na kama ni Reli yakati basi umefika mwisho Kigoma!

Kuhusiana na swala la Umri na ngono kama ulivyogusia M3 kwenye kipengele cha mwisho pia halina uhusiano na mapenzi, Ngono ni tendo linalowafanya wapenzi kuwa karibu zaidi na kujuana kiundani zaidi ukiachilia mbali suala zima la kumfanya mmoja wao kujisikia "safii" kiakili na kimwili bila kusahau kuijaza Dunia(Uzazi).

Uke wa mwanamke haubadiliki sana akizeeka (umbile) kinachotokea kwa wengi(sio wote) ni ukavu kuongezeka na hiyo huwatokea wanawake wenye umri wa zaidi ya miaka 50 au wale ambao wanaanza kukoma hedhi mapema which inaweza kuwa kwa wanawake wenye miaka 32-45(inategemea na maumbile).

Hivyo nina uhakika kabisa jamaa karidhika na alivyo jimama lake na pia inaonyesha kabisa anampenda au ni mara yake ya kwanza kupata hisia za kimapenzi (kutokana na umri wake).

Kitu pekee tunachoweza kumsaidia Dogo ni kumwambia aende taratibu (asifunge ndoa unless ni muislamu kwamba anaruhusiwa kutaliki) vinginevyo achukulie kila siku kama inavyomjia nakufurahia maisha yake ya kimapenzi na Jimama.

Atakapo kua sasa atafanya maamuzi yake ya busara na hakika akili itakuwa imetulia na kujua nini alikuwa kikifanya, anakifanya sasa na anakwenda kukifanya ktk maisha yake ya baadae.

Tuheshimu maamuzi yake na tuendelee kuwa pale kwa ajili yake atakapohitaji ushauri, tusimtupe kwa vile tu kapenda mtu mkubwa zaidi yake.

Kila la kheri!

Monday

Ufupi wangu unaudhi ndugu zake-Ushauri

Dinah habari yako nina swali nataka kujua. Mimi ni msichana nina bf tunapendana ,ila shida yangu ni hii bf wangu ni mrefu kuliko mimi. Siku moja mama yake akamwambia "unataka kuoa mbilikimo" halafu nilisikia, nilijsikia viabaya sana mpaka leo nikikumbuka ile sentensi huwa nakuwa na hasira sana.

Je niendelee kuwa naye na nivumilie "unyanyapaaji" wa ndugu zake hasa dada zake wanavyosema mimi ni mfupi au nianze zangu nikatafute mtu ambaye atanipenda na familia yake haitaniona tofauti hasa kimaumbile? Maana hata bf hapendi tuongozane maana anasema naonekana kama mtoto wake. ???

Sunday

M3 kwenye faida/hasara/umuhimu wa Ndoa!

Nilibahatika kupitia mitandao mbalimbali ili kuona maelezo mbalimbali yahusuyo mada hii. Mengi niliyoyakuta ni yaleyale ninayoyafahamu ambayo hata hivyo yameniacha nikiwa na maswali mengi badala ya majibu.

Najua dada Dinah, hata wewe umeliona hilo na kwa uzoefu wako wa kusaidia watu katika nyanja nzima ya maisha na kuridhishana kimaumbile unaweza ukatoa jibu lenye kutosheleza.

Labda nikokotoe maelezo kidogo kwanini nimeuliza hili ili kila mchangiaji aone nini umuhimu wa kufundishana na kuelezana dhana nzima ya neno ndoa, na kwanini kabla ya ndoa kuna vipengele anuai kama `uchumba’ na baada ya ndoa kuna vitu kama `fungate’ na baada ya fungate kuna nini tena?

Wengine hukimbilia `talaka’ au `misukosuko ya ndoa’ ambayo huenda imesababishwa na kutokuelewa zana nzima ya ndoa, na kwanini hii ndoa ikawepo! Wengine wamediriki kusema haina haja ya ndoa, eti kila mtu akijisikia amtafute amtakaye amalize shida zake, lakini hatimaye uzee unapotinga anajuta na anakiri kweli kuna umuhimu wa kumtafuta mwenza, ni kwanini?


Kutokana na hili nikaona kuna haja ya kutafiti kwa undani kwanini kukawa na ndoa. Hii ndoa kwanini iwe na vipengele fulani, vinasaidia nini. Na kawanini ndoa ambayo kiujuujuu tunaiona kuwa ni `raha’ ni `uhalalisho’ wa kutenda yale yaliyokatazwa, ni `kusaidiana’ kwani unaunganisha `jamii’ mbili.


Lakini kwa wengine imekuwa ni kinyume na matarajio, na wengine huishia kusema kuwa `ndoa ni ndoana’ kwani ikikunasa hunasuki. Na wachache waliofanikiwa wamekaa kimya hawataki kuwanasua walinasa kwenye ndoana hii.Tumepata maelezo mengi ya `ngono na kungonoana’ lakini hapa bado tunahitaji maelezo yanaisaidia `ngono!’


Kwani tuelewe kuwa sisi ni binadamu na tuna taratibu zilizokubalika na kututofautisha na viumbe wengine, kuwa tendo hili ni la baraka, na baraka hii haiji kama wanavyofanya wanyama.


Baraka hizi huja kwa taratibu maalumu, nayo ndiyo mchakato mzima wa kuiendea ndoa. Na hata wale waliochepuka na kuishi bila `ndoa’ hujiona hawana baraka hizi, hatimaye huamua na kusema `tunaibariki ndoa’ na ajabu kabisa, wakiamua kuibariki ndoa yao wanaumua kwenda `fungate’!.


Sasa ni kwanini ndoa, na kwanini hawa waliamua kuibariki ndoa yao bado wanakimbilia kufanya fungate na ili hali walishapimana vya kutosha?Hili linahitaji uwanja mpana wa maelezo.

Ninaomba dada Dinah, ulikuze na uliwekee vipengele ili tujifunze, sio sisi tu tulio ndani ya ndoa lakini hasa vijana wetu wanajiandaa kuingia katika uwanja huu mpana wa `mke na mume’, ili wasije wakataabika, na kuishia kuchukiana badala ya `kupendana’ na baya zaidi tunaweza tukapunguza tatizo kubwa la gonjwa la `ukimwi’ kama kweli tutakuwa tumefuatilia kwa namna yake utaratibu huo mzima wa ndoa na kabla na baada.

Kama nimekosea tusahihishane.

Mimi emu-three

Ignorant kwenye Hasara,Faida,umuhimu wa ndoa.


Ignorant, mchango wako umenifurahisha sana.

"Kwanza kabisa, pamoja na sababu ya mada hii kupata... Kwanza kabisa, pamoja na sababu ya mada hii kupata wachangiaji wachache kama ilivyotolewa na M3, nadhani urefu wa maelezo ya DL nayo pia ni inachangia kupata wachangiaji wachache.


Sidhani kama watu wengi wanaoingia hapa wamesoma post yote, na kama ndiyo, wachache wanaweza pata wazo la kuchangia baada ya kusoma post ndefu kama hii. Ok, nirudi katika mada yenyewe.Kwa mtazamo wangu, maelezo ya wachingiaji hapo juu yana-reflect jinsi tulivyokuzwa kuamini ngono ni mbaya.


Mbali na hilo, maelezo mengi yanachanganya madhumuni ya ngono na ndoa kuwa kitu kimoja. Nitaeleza haya.Tukiweka imani za kidini pembeni, (kwani mambo mengi ya kidini huwa hayajadiliki kutokana na kuwepo kitu utakatifu na hivyo kutompa binadamu yeyote uwezo wa kukosoa au kujadili uhalali wake).


Kwa mtazamo wangu, ngono ni kitu tofauti kabisa na ndoa. Ngono ni tendo la kukutanisha sehemu kike na kiume ilhali ndoa ni makubaliano ya watu wawili kuishi pamoja na inatarajiwa watu hawa kua jinsia tofauti (ingawa siku hizi kumeingia aina mpya ya ndoa). Kwa mtazamo huu, hailazimishi vitu hivi viwili kuendana kwa pamoja au kuuliza kipi kianze na kingine kifuate ingawa inajulikana kua katika ndoa kutakua na ngono.


Kutokana na makuzi yetu, mambo haya mawili yamewekwa pamoja na hivyo kuzua utata katika kutambua kila kimoja wapo. Kuchanganya kwa madhumuni ya kingono na ndoa ndiyo yanasababisha wanawake wengi kudhani wamedanganywa na wanaume pindi wanaposhindwa kuolewa ilhali wameshangonoana na hao wanaume (same men).


Kwa upande mwingine, wanaume nao wanakua waongo kwa kuahidi ndoa kwa wanawake/wapenzi wao ili wapate ngono. Kama ngono na ndoa vingeeleweka kua ni vitu viwili tofauti, maumivu na uongo huu usingetokea. Suala la kudhalilisha utu/ubinadamu kwa kuonyesha uchi/utupu linahitaji mjadala zaidi.


Suala la kudhalilika kwa kuonyesha utupu linategemea sana jinsi mtu alivyokuzwa kama sio utamaduni. Napenda nipingane na maelezo kua ngono hudhalilisha mtu kwa kua anaifanya akiwa mtupu, tunaweza kusema nini kwa wale madaktari walio na mwanya wa kuona utupu wa wagonjwa wao? Vp udaktari nao unadhalilisha utu?Kwa kumalizia, naomba tusome alama za nyakati.

Tuangalie ni nini kinawezekana kwa nyakati hizi na pengine kutambua mabaya na mazuri yake na jinsi ya kupunguza athari za hayo mabaya. Suala la kujadili ngono kabla ya ndoa ni bora au la ni la msingi, hata hivyo kwa kuangalia kinachoendelea katika jamii, ni vizuri tukafikiri zaidi ya swali hili. Sidhani kama watu wanaofanya ngono kabla ya ngono hawafahamu faida na hasara zake.

Tujadili yale tunayoweza kuyafanyia kazi."

Wednesday

DL kwenye Umuhimu/faida/hasara ya ndoa.


DL nafurahishwa na michango yako!


"Dear Dinah,
Naomba unipe nafasi nitoe maoni yangu machache kuhusu maudhui ya hapo juu.Siyo rahisi kutoa jibu moja kuhusu tendo la ngono kabla au bada ya Ndoa kama ni sahihi au afadhali au ni vyema au si sahihi au si vyema.


Tatizo kubwa linatokana na mambo mawili: Imani za kidini au miko ya kijamii, kwa upande mmoja, na lengo la wanaotaka kufanya kitendo hicho ni nini hasa, kwa upande wa pili.
Kwa upande wa imani za kidini –na hapa karibu dini zote, hasa Dini Samawiya (Dini za Vitabu Vitakatifu kutoka Mbinguni)- au hata miiko ya kijamii, ngono kabla ya ndoa inakatazwa –haramu- na ni mwiko kwa jamii, yaani marufuku.


Upigwaji marufuku huu unatokana na mtazamo wa kina wa dini na jamii mbali mbali kuhusu madhumuni hasa ya ndoa. Madhumuni ya ndoa, kidini na kijamii, ni kuendeleza na kutunza vizazi vya jamii (re-creation) kupitia ahadi (ndoa), mbele ya mashahidi kwamba ahadi hiyo itaheshimiwa na kutekelezwa chini ya taratibu zilizowekwa, kwa msingi wa upendo, uvumilivu na uungwana, mambo ambayo ndiyo mihimili ya Mapenzi (Love) .


Hivyo, madhumuni makubwa ni kuendeleza na kutunza kizazi; yaani matunda ya ndoa, ambayo ni watoto na familia. Raha na utanashati (recreation) na mapenzi (love), kwa maana hiyo, ni malengo ya pili, au ni matokeo ya lengo kuu la kwanza la ndoa: yaani kuendeleza vizazi.


Kwa mtazamo huo, basi, hapana mjadala kwamba ngono kabla ya ndoa, hata kama inatokana na pendo au mapenzi, haikubaliki; maana inakosa uhalali (leseni) wa jukumu la msingi la kuendeleza kizazi cha jamii (re-creation) mbele ya mashahidi. Raha na starehe (recreation) ni matokeo na natija ya madhumuni hayo halisi.


Ndoa, kwa maana hiyo, ni mapatano ya msingi ya utekelezaji wa ahadi. Kwa maana hiyo, ndoa lazima ije mwanzo kabla ya ngono na si venginevyo. Ukiacha maadili ya kidini na kijamii, na ukayaweka kando, na ukajiuliza je ni afadhali au si afadhali kufanya ngono kabla ya ndoa, basi bado hutaweza kupata jibu la haraka, hata wewe mwenyewe, kama hujajiuliza swali la msingi kabisa, kwanza.


Nalo ni hili: Nini hasa madhumuni ya ngono unayotaka kuifanya? Ni raha na starehe tu au ni raha na starehe pamoja na yanayoweza kutokana na raha hizo na starehe hizo? Ikiwa madhumuni makubwa ni raha na starehe (recreation) inayoweza kupelekea kupeyana ahadi (ndoa) kuhusu kuendeleza na kutunza kizazi basi unaweza kusema kwamba ngono kabla ya ndoa ni jambo la maana; maana inatoa mwanya mzuri wa kupima tabia, uelewano, uvumilivu na hata kiwango cha pendo au mapenzi, kwamba je upo uwezekano wa kufungamana kwa muda mrefu?


Ni pima maji; je unaweza kuyavulia maji nguo na kuyaoga au la? Lakini, na hapa napenda kusisitiza LAKINI laima nyote wawili muwe wakweli; wakweli kwenye nia yenu hiyo na si venginevyo.

Venginevyo mtakuwa, ama nyote wawili mnajidanganya, au mmoja wenu ambaye si mkweli anajidanganya na kumdanganya mwenziwe. Lakini ikiwa madhumuni halisi ni raha na starehe TU, basi ngono ndiyo tendo kuu la kutoa kiu hicho cha raha na starehe hiyo. Ila, kwa nanma ilivyo, ni jibu la muda tu. Suala la ndoa halipo wala halifikiriwi. Hapa wapo watu wa aina mbili.


Kuna wale ambao wanatafuta raha na starehe tu na si jambo jengine. Kila mmoja anatafua kukata kiu chake tu.Wengine ni wale ambao wanatafuta raha na starehe hata kwa kununua au kuuza miili: ambao jamii huwatambua kuwa ni malaya na wahuni. Miongoni mwa wahuni unaweza hata kukuta “wana ndoa”.


Makundi yote haya mawili yanayowinda raha na starehe tu yanachangia sana matatizo ya kusambaza maradhi mbali mbali, miongoni mwao wenyewe kwa wenyewe na miongoni mwa jamii zao na jamii za wengine. Wanaweza hata kuathiri familia zao wenyewe, kwa wale ambao wameshaoa au kuolewa.


Pale lengo la raha na starehe linapokumbana kiajali tu na uja-uzito, au kunogewa na fungamanisho la ngono, basi wana-ngono hao huanza kufikiria njia mojawapo ya ama kujipa majukumu ya matokeo hayo, au ya kuwatangazia wengine kwamba wawili hao ni wao-kwa-wao hawataki mshirika nao. Mojawapo wa njia za lengo hilo ni ndoa.


Nyengine ni Unyumba, au kuishi-kimada na kadhalika. Kwa vizazi vya siku hizi, u-BF-GF au wapendanao, ni mojawapo wa njia hizo. Hawa wa siku hizi, wanasaidiwa sana kufikisha malengo yao hayo na vidonge vya kuzuwiya uzazi. Ngono kwa hawa ni lengo la raha na starehe. Endapo watanogewa na kuelewana basi wanaweza kufunga ndoa.


Venginevyo, kila mmoja anafunga virago vyake na kuelekea kwengine, na kuanza upya. Hivyo, narudia kusema kwamba si rahisi kutoa jibu la mkato au jibu moja, kabla ya kujuwa madhumuni halisi ya tendo hilo la ngono. Ila naweza kusema kwamba ni afadhali sana na ni busara kubwa ndoa kuitangulia ngono na si kinyume chake.


Yaani ni bora kumtafuta wa kuishi naye kwa mapenzi kabla ya kufanya mapenzi yenyewe. Na hapo ndipo penye tofauti kati ya ngono na mapenzi. Ngono inaweza kukata kiu lakini haishibishi. Mapenzi yanakata kiu na yanashibisha. Ngono inatoa raha ya muda.


Mapenzi yanatoa raha ya muda mrefu. Ngono inapapatisha amani na utuilivu wako, na kupoteza vyako, na pengine hata vya wenziwako.Mapenzi yanadumisha amani na utulivu wako, pamoja na kutunza vyako na hata vya wenziwako.

Mwenye akili haambiwi chagua. Mwenye macho haambiwi tazama. Mwenye masikio haambiwi sikia. Kila kitu kiko wazi kama giza la usiku na anga la mchana.
Upo hapo?!!!" DL.

Monday

M3-Faida/Hasara na umuhimu wa ndoa!

M3 michango yako inanifurahisha sana kaka. Shukurani!

"NDOA ni muhimu na ina faida na hasara zake `Je ni vyema tukasubiri hadi tufunge ndoa ndipo tungonoane au ni vyema `tukapimana’ kwanza ili baadaye tukifunga ndoa tuwe tumejuana vyema? Na kama ni hivyo ina maana gani ya kufanya `fungate’.

Nini hasa FUNGATE, Ina umuhimu katika ndoa? Naomba utusaidie zaidi katika haya. N.B Hapa wengi tunashindana tunaposikia hoja ya kuwa `ndoa’ na ngono ni vitu viwili tofauti naya kuwa Ndoa ni mjumuiko wa vitu vingi ikiwemo ndoa.

Ni sawa kutegemeana na imani zetu, lakini zipo imani zingine `ngono’ hairuhusiwi mpaka ndoa, kwahiyo ngono ni kipengele muhimu kuliko mambo mengine. Hapa napo unasemaje?

Na kama ulivyosema ni vyema kuishi kimaadili na kiimani. Kimaadili na kiimani nijuavyo mimi, nikukwepa kabisa swala la ngono hadi ndoa itimie kama sikosei, sasa katika hoja tulizoshauriana hasa zile zinazowahusu `wapenzi’ kuwa mfanye hivi na vile.

Hawa je siwanafanya ngono nje ya ndoa, je kipindi hicho wakiwa wanafanya hivyo nje ya ndoa , kuna tofauti gani waliyoiona baada ya kuoana?

Hili lilikuwa swali la awali na nafikiri majibu tumeyapata. Basi katika mada zako zijazo pia utusaidie kutuelezea umuhimu wa `imani’ katika `ndoa’ au mapenzi kwa ujumla. "

Ahsante tena emu-three

Friday

Kwanini W'wake pesa mbele mapenzi nyuma?

Imefikia wakati sasa nimekata tamaa, Dinah na wadau wengine mnajua kuwa ndani ya miaka saba kila mwanamke niliempenda na kuanzisha nae uhusiano anaonyesha kuipa pesa kipaumbele kuliko hisia za kimapenzi.

Awali nilidhani ni ugumu wa maisha kwa baadhi yao lakini nikaja kugundua hata wale mabanti waliotoka kwenye Familia zinazojiweza bado wanakuwa na hii kasoro ya kuthamini pesa zaidi kwenye uhusiano kuliko mapenzi yenu.

Je ni kasumba kuwa ukiwa na mwanaume ni lazima pia uwe mchimbaji wa dhahabu au ni nini hasa?

Imefikia wakati sasa naogopa kuanzisha uhusiano kwa vile nahisi hakuna atakae nipenda na kunipa penzi la kweli kama nifanyavyo mimi bali atakuwa na mimi ili kupata kile kidogo nilicho nilichonacho.

Jawabu: Shukurani kwa kuleta mchango wako hapa ulio katika mfumo wa swali. Hili suala nimekuwa nilisikia sana tangu nakua mpaka leo nimekomaa. Tena ni juzi tu nimetoka kuongea na Rafiki mmja akawa anasikitika kuhusu hili, hali inayofanya nitambue kuwa limekuwa tatizo kubwa kwenye jamii.


Inawezekana kabisa ikawa ni sehemu ya Asili ya mwanaadamu kuwa Mwanaume mtafutaji/mwindaji na Mwanamke mzazi na mlezi, lakini kutokana na maendeleo tuliyonayo hali imebadilika na sasa tunashrikiana na kusaidiana ktk kila jambo.

Kasumba ambayo imejengeka/zoeleka kuokana na mfumo dume inaweza kuchangia tabia hii kwa baadhi ya wanawake, vilevile kuna uwezekano kuwa ni mazoea yaliyobadilika na kuwa tabia na sasa imekuwa kama sehemu ya "Utamaduni" au niseme maisha ya baadhi ya wanawake kwa kisingizio cha "ugumu wa maisha".


Pia baadhi ya wanaume wanachangia hii tabia kuota mizizi na kuwa kasumba na hatimae "Utamaduni" (kama nilivyosema hapo juu) wa wanawake wengi kutokana na kitendo cha kutumia pesa kama "fimbo" au nyenzo ya kupata mwanamke.

Wapo baadhi ya wanaume ambao hujiona "Baba" kwa wapenzi wako (hasa kama ni wakubwa kiumri), kila ukikutana nae lazima akuachie "kitu kidogo" akisema nauli au kanunune soda.

Hii tabia wanayo akina baba wazazi (well baba'ngu miaka ile) mkipanga mihadi na kukutana lazima atakushikisha senti kabla hamjaachan akisema nunua kitu utakacho huko njiani.

Sasa Binti aliyezoea shikishwa Laki moja ya "nauli" na Mpenzi ajionae "baba" mara uhusiano huo ukiisha itakuwa ngumu sana kwake kuvumilia uhushiano mwingine bila kupewa pesa ya "nauli" kwa hiyari, na matokeo yake ama atahisi hapendwi (Kisaikolojia atakuwa akidhani kupendwa na mwanume ni kupewa pesa) au ataanza kukuomba kila mkikutana.


Kinachosikitisha zaidi kwenye hili suala ni kuwa Wanaume wengi wanapenda kujionyesha na "kujisigizia" mali ambazo hawana ilihali "kum-wow" mwanamke ili kushawishika kirahisi na akifanikiwa kumpata mwanamke husika Bwana atajitahidi kwa hali na mali ili aweze kuendeleza aina ya maisha fulani ambayo ameyaanzisha sambamba na uhusiano wake.

Hapo ni wazi kuwa uhusiano utaegemea kwenye ulichotumia kumshawishi (pesa/mali) na sio penzi kwani kilichomvuta kwako ni "misifa" na sio penzi au mvuto wao kwake japo kuwa wewe ulimpenda kimapenzi.


Kitu kingine ningependa kuongezea kwenye kujibu swali lako ni kuwa wanawake wengi wanapenda kusingizia ugumu wa maisha kama fimbo ya kupata senti kutoka kwa wanaume, na wanasahau kuwa ugumu wa maisha ni kwa kila mtu na sio Jinsia moja tu.


Mwanaume pia anakabiliwa na ugumu huohuo wa maisha lakini inakuwaje yeye anapata hata hicho kidogo chakukugawia wewe wanamke na wewe usipate ili mchange na kuwa na mahela ya kutosha kuendesha maisha kwa pamoja kama wapenzi?

Natambua pesa ni muhimu sana ktk maisha yetu ya kila siku na ni vema kuwa kwenye husiano ambao unajua kabisa utakuwa umelindwa kiuchumi, kihisia, kimwili n.k. incase of anything kama Mimba, kuugua namenginemengi ya kibinaadamu.

Pamoja na kusema hivyo ukubali ukweli kuwa unapoingia kwenye uhusiano unaingia kwa vile unampenda huyo mtu na unataka uchangie maisha yako na yake kwa ukaribu zaidi, mshirikiane kwa kila jambo.

Kidokezo

Penzi ni hisia na sio pesa au chochote kinachohusisha pesa. Kwa kumalizia tu napenda kusema kuwa ni vema unapomtokea mtu umtokee kwa kumueleza hisia zako za kimapenzi juu yake.

Ule mchezo/tabia ya kutongoza mabinti kwa kuwaahidi maisha mazuri, kuwapeleka popote watakako, kuwanunulia watakacho muiache. Wakati umefika kwa wanaume kuwa wazi na kuachakutumia pesa/uwezo wenu wa kimaisha ili kumshawishi mwanamke.

Just be yourself au a bit humble kama mambo yako safi na utakumbana na penzi la kweli lisilojali ulichonacho bali hisia zako tu.

****Samahani kwa kiswahili changu cha ovyo....Asante.

Wednesday

Samahani!

Kwa kupotea ghafla, "nilibanika"(busy) na majukumu ya kulinda ndoa, si wajua ukijisahau kidogo inakubidi urudi kwenye "basics"? Basi ndio hivyo ilivyokuwa.

Ila sasa mambo yatakuwa bomba, endelea kuwepo ili tujifunze pamoja.

Pages