Tuesday

Nafasi ya Wife, Unapogundua mtoto si wako-Ushauri

"Mie nafurahia sana jinsi unavyosaidia watu sijui ni kipaji au ulisomea haya mambo ya kushauri watu. Leo na mie natoa uzoefu wangu wa maisha ya ndoa naamini kuwa utasaidia wanablogu hii na wasomaji wengine kuwa makini na wapenzi wao.

Mie nimeolewa miaka saba iliyopita na tumebarikiwa kupata watoto wawili. Wakati tunachumbiana na mume wangu aliwahi kuniambia kuwa alizaa na mwanamke mwingine na waliachana miaka michache kabla hajakutana na mimi.

Ukweli sikujisikia vizuri kuwa na mwanaume aliyezaa na mwanamke mwingine lakini alinihakikishia kuwa haikuwa wazo lake kuzaa na yule mwanamke ila mwanamke yule alijilengesha ili Mume wangu asimuache wakati ule wako pamoja. Nilijitahidi kumuamini lakini bado nyuma nilikuwa nasumbuliwa na maswali kibao.


Mume wangu hakuwa akijihusisha sana na mwanamke yule isipokuwa kama mtoto anahitaji mahitaji muhimu ambayo yule mwanamke hawezi kutimiza au kama mtoto anaumwa, basi mume wangu akiwa kwenye heka heka za kumshughulikia mtoto wake mimi nilikuwa naumia sana nikifikiria mambo mengi ya kimaisha na uhusiano kati ya watoto wetu na mtoto huyo wa nje ya ndoa wa mume wangu.


Siku moja nikamuomba mume wangu amlete mwanae hapa nyumbani ili ajenge uhusiano na wanangu, lakini mume wangu alikataa kwa madai kuwa ni mapema kwake kufanya hivyo. Nilimuelewa na nikaheshimu uamuzi wake. Siku zikapita na sasa inakaribia mwaka mume wangu hajagusia lolote kuhusiana na mtoto wake huyo wala mama wa mtoto huyo kama ilivyokuwa zamani.

Juzi juzi hapa basi tukapata wageni kutoka upande wa mume wangu, kwa bahati nzuri tunaelewana sana na tunaongea mambo mengi tu kuhusu maisha. Mmoja kati ya mawifi zangu akagusia kuhusiana na mtoto wa nje wa mume wangu akaniuliza kama najua kuwa mume wangu alizaa nje. Mie nikajifanya kuwa sijui ili nipate umbea zaidi manaa yake wao walikuwepo na kaka yao na huyo mwanamke kabla mimi sijatokea kwenye maisha ya kaka yao.

Wifi yangu alizungumza mambo mengi ya kutisha na kusikitisha kuhusiana na uhusiano wa kaka yake na mwanamke aliyezaa nae. Kilichonitisha ni mwanamke yule kwenda kwa mganga ili mume wangu wakati huo alikuwa bwanake wafunge ndoa.

Wifi alinisimulia harakati zote walizozifanya mpaka kumpeleka kaka yao kwenye maombi na kufanikiwa kumtoa kaka yao kwenye maisha ya mwanamke yule na mwaka jana wakaamua kufunga safari na mtoto yule mpaka Afrika ya Kusini na kufanya vipimo vya DNA na kugundulika kuwa mtoto yule kumbe hakuwa wa damu wa mume wangu.

Baada ya maelezo hayo nikakumbuka safari ya mume wangu kwenda Afrika kusini kwa wiki moja na aliporudi alikuwa kama mgonjwa mie nikadhani ni uchovu wa safari. Pia nikagundua kwanini mume wangu alikataa kumleta mtoto yule pale nyumbani na kwanini siku hizi hazungumzii kuhusu huyo mwanamke wala mtoto wake wa nje.

Nashukuru Mungu nimejua ukweli kuhusu lakini nasikitika na kushangazwa na kitendo cha mume wangu kukaakimya kipindi chote cha mwaka mzima bila kunieleza lolote juu ya DNA au kuniambia tu kwa kifupi kuwa yule mtoto sio wake. Kwanini ananichunia kuhusu suala hilo wakati mwanzo alinihusisha?

Je itakuwa sahihi kama nitamuuliza? Kama ndio je nitaanzaje kuuliza ili aseme mwenyewe badala ya yeye kuja kugundua kuwa dada yake ndio aliyetoboa siri kwangu?

Mwenzeni hapa nilipo sielewi nini cha kufanya pia namuonea huruma mume wangu kwani najua kabisa anaumia na kujuta ndani ya moyo wake kutokana na muda alioupoteza kwa mtoto yule.
Mrs Mwilima, Dar es Salaam."

Dinah anasema:Mama Mwilima shukrani zikufikie kwa ushirikiano wako. Mimi binafsi sidhani kama ni sahihi kwa wewe kumuuliza mumeo kitu ambacho hakipo tena kwenye maisha yake. Hata mimi nahisi kuwa Dada mtu ambae ni wifi yako alitumwa na familia ya mumeo kukueleza wewe ukweli huo ktk mtindo wa siri, hii inawezekana ni ktk harakati za kuzuia mumeo kuumia zaidi kwa kujibu maswali mengi zaidi kutoka kwako kama mkewe (una haki zote za kujua kila kitu kuhusu mumeo).

Nini cha kufanya:Sahau kuwa mumeo alikuwa na mtoto kwani imejulikana sio wake, hivyo hakuna sababu ya kushupalia kitu ambacho hakipo tena na badala yake zingatia hali ya sasa ya mumeo. Natambua mumeo anahitaji muda ili kupona maumivu hayo (mwaka mmoja hautoshi kuponya maumivu yaliyowekwa kila siku ndani ya miaka yote aliyoishia kidhani mtoto ni wake), na wewe mkewe ndio mtu pekee utakaefanikisha uponaji wake wa haraka ili wote kwa pamoja muanze kuishi maisha yenye furaha na amani kama zamani.

Mpe ushirikiano mumeo, muonyeshe mapenzi ya kihisia zaidi na kumjali ktk kipindi hiki kigumu cha kukabiliana na masumbufu ya Kiakili na Kisaikolojia usikute hata Kiuchumi kwani Miaka yote hiyo alikuwa akipenda, kujivunia, kujali na akihudumia mtoto wa mwanaume mwingine akidhani ni wake.

Wewe pia unatakiwa kuwa mvumilivu kwani kipindi hiki mumeo anaweza akawa na hofu juu ya watoto wenu hao, inawezekana kabisa akawa anajiuliza mara nne-nne kama kweli ni wake au analelea mtu mwingine?

Ukiona hali yake inaendelea kuwa hivyo basi nakushauri wewe na wanafamilia kushirikiana na kumtafutia msaada wa Therapy ili kukubali ukweli, kusahau yaliyopita ili aweze kuendelea na maisha yake.

*****Haya mambo yapo sana na yanasikitisha lakini ukweli unabaki pale pale kuwa mama ni mtu pekee anaejua baba wa mtoto, Mtu unapoambiwa "huyu mwanao/mwanangu" Kisaikolojia watu wanaweza kuona mtoto kafanana sana na wao au babu, bibi, baba, shangazi yake n.k. lakini ukweli ni kufanya hiyo DNA Test kama unawasiwasi.

Kila la kheri Mrs Mwilima.

No comments:

Pages